TALIRI YATAKIWA KUFANYA TAFITI ZITAKAZOLETA TIJA SEKTA YA MIFUGO


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, (Mifugo), Prof. Elisante Ole Gabriel ameiagiza Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), kufanya tafiti zitakazo lisaidia taifa kupiga hatua kupitia sekta ya mifugo.

Prof. Ole Gabriel, aliyasema hayo wakati wa kikao cha baraza la wafanyakazi wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), kilichofanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri ya jiji Mkoani Dodoma Aprili 23, 2021.

Akizungumza na Wajumbe wa baraza hilo Prof. Ole Gabriel alisemakuwa, hakuna Taasisi nyingine ambayo Wizara hiyo inaweza kuitegemea katika suala la utafiti zaidi ya TALIRI, hivyo ni lazima ifanye tafiti zitakazo boresha sekta ya mifugo nchini na kuchangia pato la taifa.

Tusibakie kujisifu tuu kuwa Tanzania ni nchi ya pili barani Afrika kwa idadi kubwa ya mifugo lazima tujisifie kwa namna tutavyoweza kutumia sekta hii kukuza uchumi wa taifa” alisema Prof. Ole Gabriel

Alisema kuwa tafiti ndizo zinaweza kulisadia taifa kutoka hapa lilipo na kupiga hatua kufikia nchi ambazo zimefanikiwa katika sekta ya mifugo.

Kama Rais alivyokuwa akitoa hotuba yake bungeni alisema ng'ombe wetu akichinjwa nyama yake haiwezi kuzidi kilo 150 hii yote ni kutokanana kutokuwa na utafiti wa mbegu bora ambazo zitaweza kutoa kiasi cha kutosha cha nyama” alisema Prof. Ole Gabriel

Aidha alisema kuwa, TALIRI inatakiwa kufanya tafiti ya mbegu bora za ngombe ili kuwa na uhakika wa nyama ya kutosha pamoja na maziwa.

Lazima sekta hii ya mifugo tui ‘link’ na Tanzania ya viwanda hivyo basi tunatakiwa kuhakikisha kuwa ng'ombe wetu wanatoa nyama ya kutosha na iliyo bora, maziwa mengi, ngozi, pembe pamoja na kwato” alisema Prof. Ole Gabriel

Kadhalika alisema kuwa kama sekta ya mifugo itashindwa kuwa na bidhaa zitokanazo na mazao ya mifugo bora, hata malighafi kwa ajili ya viwanda hazita kidhi viwango.

Aliongeza kuwa ni wakati sasa kwa Taasisi hiyo kukaa mguu sawa silaha begani ili kuzalisha mifugo bora na kukuza sekta ya mifugo.

Vile vile, aliiagiza TALIRI kuhakikisha wanakuwa wabunifu katika kuangalia changamoto mpya zinazohusu wafugajiili kuzifanyia kazi mara moja.

Kwa upandewake Mwenyekitiwa baraza hilo na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TALIRI Dk. Jonas Kizima, alisema kuwa kikao hicho ni cha pili kwa baraza hilo na moja ya kazi yake ni kupitia bajeti yake.

Pamoja na kupitia bajeti pia mweshimiwa Katibu Mkuu tutakuwa na maazimio ambayo tutayaandika na kukuletea wewe ikiwa ni sehemu ya utekelezaji" alisema Kizima.

Kwa upande wao Wajumbe wa baraza la wafanyakazi TALIRI wamemshukuru Katibu Mkuu (Mifugo) kwa kuweza kufika na kushiriki nao nakuahidi kuwa wamepokea maelekezo yake na watahakikisha wanayafanyia kazi na kuyasimamia vizuri Ili kuongeza tija na ufanisi katika kazi zao za kitafiti.

Post a Comment

0 Comments